728x90 AdSpace

  • Latest News

    Wednesday, June 01, 2016

    SERIKALI YASHTUKIA HUJUMA YANGA SC


    SERIKALI imeliagiza Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kumtumbua ofisa wake anayehujumu uchaguzi wa Yanga kabla wao hawajamchukulia hatua kali.
    Akizungumza jana, Katibu Mkuu wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Mohammed Kiganja alisema uchaguzi wa Yanga upo kama ulivyopangwa awali, ingawa kuna baadhi ya watu wanadaiwa kufanya hila za makusudi kukwamisha uchukuaji wa fomu kwa kushirikiana na Ofisa wa TFF.
    “Uchukuaji wa fomu ulishaanza, lakini wapo watu na kwa bahati mbaya wengine wamo ndani ya TFF na wengine wako nje wanahangaika kuhakikisha uchukuaji fomu haufanikiwi,” alisema Kiganja na kuongeza: “Huyu mtu sisi tunamjua, na kuna baadhi ya watu wamekwenda pale kwa lengo la kuchukua fomu wakanyimwa kwa kigezo Jumamosi na Jumapili sio siku za kazi, bahati mbaya zaidi hata kwenye mtandao hawakuweka mpaka tulipowakoromea jana (juzi), ndio wameweka, “ alisema.
    “TFF imchukulie hatua haraka iwezekanavyo ofisa huyo kabla sisi hatujamchukulia hatua,” alisisitiza Kiganja na kuongeza kuwa bado wanawasaka wengine wa nje, ambao wanashinikiza uchaguzi usifanyike. “Nia ya serikali kuona klabu, vyama na mashirikisho yote ya michezo wanaheshimu sheria, kanuni na katiba zilizopo.”
    Kiganja, akizungumzia ombi la wazee wa Yanga la mkutano wa dharura alisema; “ “Hakuna mkutano wa dharura waende kwenye uchaguzi, walikuwa wapi siku zote mpaka wasubiri serikali iitishe uchaguzi ndipo watake mkutano, walete kimaandishi na hata wakileta hatuwapi kibali.....Kama wanampenda sana Manji wamwambie achukue fomu waende kwenye uchaguzi wamchague kwa kura za kishindo,” alisema.
    Mwishoni mwa wiki Baraza la Wazee wa Yanga, kupitia kwa Katibu wake, Ibrahim Akilimali waliiangukia TFF na BMT kuwaruhusu wafanye mkutano wa dharura wajadili uchaguzi wao ikiwa ni pamoja na kuwapa muongozo wa kadi zitakazotumika kwenye uchaguzi wao.
    Aidha, Kiganja aliwataka wadau wajitokeze kuchukua fomu za uongozi ndani ya klabu hiyo na kwamba uchukuaji fomu ukiendelea kusuasua, BMT italazimika kuvunja sekretarieti nzima ya Yanga na kuunda kamati ya mpito itakayofanya kazi ndani ya miezi mitatu ikiandaa uchaguzi mpya.
    Naye Ofisa Habari wa TFF, Alfred Lucas alisema huenda uchukuaji fomu ukasogezwa mbele kwa siku mbili zaidi na kwamba Kamati ya Uchaguzi ilitarajiwa kukaa jana jioni kuzungumzia uchaguzi huo ambao umepangwa kufanyika Juni 25.
    Uchukuaji wa fomu ulianza Mei 24, mwaka huu na kufikia jana ilitarajiwa orodha ya wagombea ingekuwa imepatikana kabla ya kuanza kwa taratibu nyingine kuelekea uchaguzi huo.
    Ukomo wa uongozi wa Yanga chini ya Yusuf Manji ulikuwa Juni 2014, lakini wanachama waliridhia kumuongezea mwaka mmoja kwa kile walichodai aweze kukamilisha baadhi ya mambo ambayo alikuwa hajayakamilisha.
    Hata hivyo, muda wa nyongeza huo wa mwaka mmoja ulimalizika Juni mwaka jana, lakini ukimya juu ya uchaguzi mkuu ulitawala hadi Serikali kupitia BMT ilipoingilia kati na Aprili 19 kuiagiza TFF ihakikishe Yanga inafanya uchaguzi wake ndani ya siku 72.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Post a Comment

    Item Reviewed: SERIKALI YASHTUKIA HUJUMA YANGA SC Rating: 5 Reviewed By: Unknown
    Scroll to Top