728x90 AdSpace

  • Latest News

    Thursday, May 26, 2016

    YANGA SC KUONDOLEWA CAF

    Dar es Salaam,Tanzania.

    KUNA kila dalili za Klabu ya Yanga kuondolewa kuwa mwanachama wa Shirikisho la Soka barani Africa (CAF) endapo itaendelea kukaidi kufanya uchaguzi mkuu kama ilivyoagizwa na Serikali kupitia Baraza la Michezo Tanzania (BMT).

    Akizungumza jana, Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi TFF, Aloyce Komba, alisema kwamba zoezi la kuchukua fomu kwa wagombea ilikuwa lianze jana, lakini limeshindikana kutokana na uongozi wa Yanga kukaa kimya na kuvuruga ratiba yote kama ilivyopangwa.

    “Kuna dalili za uongozi wa Yanga kuhujumu uchaguzi huo usifanyike kwani mpaka sasa wamevuruga ratiba ya uchaguzi huu na tayari tuliwapa mfano wa fomu za uchaguzi huo ili zitengenezwe na kisha kurejesha TFF, lakini mpaka (leo) tunaona kimya na hawajasema lolote,” alisema Komba.

    Komba ambaye pia ni Mwanasheria alisema kuwa kipindi hiki ambacho timu ya Yanga inashiriki kwenye mashindano ya kimataifa, ilitakiwa kufanya uchaguzi kwani wanaweza kufika mbali na moja kati ya timu ikabaini kwamba wameondolewa na timu ambayo si mwanachama wa CAF wanaweza kuondolewa.

    “Yanga inashiriki mashindano ya CAF na shirikisho hilo likigundua kwamba viongozi wake hawapo kihalali madarakani na haina leseni ya klabu inayolitambua, inaweza kuondolewa na kuwa pigo kubwa kwao,” alisema Komba.

    Mwenyekiti huyo wa Kamati ya Uchaguzi TFF alisema kuwa shirikisho hilo limeshaziagiza klabu nchini kukamilisha taratibu za kanuni mpya ya Leseni za Klabu (Club Licensing) na vijana hao wa Yanga mpaka sasa hawana leseni ya CAF, hivyo Watanzania wasishangae watakaposikia imeondolewa kwenye Kombe la Shirikisho.

    Komba alisema kuwa mvutano wa uchaguzi unaotaka kufanyika sasa utapelekea CAF kushtuka na kuja kufanya ukaguzi wa siri kwa lengo la kubaini kama klabu za hapa nchini zina sifa za kuitwa klabu za Ligi Kuu bila kuwa na leseni yake.

    Aidha, Komba alisema kwamba kamati yake inatarajia kutoa tamko lake leo juu ya hatima ya uchaguzi huo baada ya uongozi wa Yanga kukaidi kutekeleza kama Serikali ilivyoagiza.

    TFF hivi karibuni ilitangaza uchaguzi mkuu wa Klabu ya Yanga kuwa ufanyike Juni 25, mwaka huu badala ya Juni 5 iliyokuwa imepangwa hapo awali. Kwa mujibu wa ratiba ya TFF, fomu za kuwania uongozi wa Yanga zilitakiwa kuanza kuchukuliwa Mei 25 mwaka huu jambo ambalo limeshindwa kufanyika.

    Serikali iliitaka klabu hiyo kutumia katiba ya mwaka 2010 na kwamba wanachama wa Yanga watatumia kadi za kawaida za uanachama na si za benki. Juhudi za kuwapata viongozi wa Yanga kuzungumzia suala hilo ziligonga mwamba kutokana na simu zao kuita bila kupokelewa.

    CHANZO:BINGWA
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Post a Comment

    Item Reviewed: YANGA SC KUONDOLEWA CAF Rating: 5 Reviewed By: Unknown
    Scroll to Top