728x90 AdSpace

  • Latest News

    Friday, October 31, 2014

    SIMBA BADO SIYO SHWARI

    SARE tano ilizopata Simba katika mechi
    zake za kwanza msimu huu zimeibua
    mambo na sasa baadhi ya vigogo wa
    Yanga wameweka wazi kwamba tatizo la
    Wekundu hao ni mipango yao inavuja
    wala si hujuma.

    Mmoja wa viongozi wenye ushawishi
    mkubwa ndani ya Yanga na ambaye
    anajulikana kwa rekodi zake za
    mapambano, ameiambia Mwanaspoti
    kwamba tofauti za kimisimamo baina ya
    viongozi wa juu zinachangia mambo
    mengi ya ndani kuvuja na kuwapa wao
    faida ndio maana mambo
    yanawanyookea.

    “Tunajua kila kitu kinachoendelea Simba
    kwani wengine ni rafiki zetu hivyo huwa
    wanatuambia nini kinafanyika katika
    uongozi, kuna baadhi ya viongozi ambao
    kwa sasa wamekaa pembeni na wana
    urafiki mkubwa na baadhi yetu hivyo
    huwa wanashirikiana mambo mengine
    ikiwemo kujua siri za Simba.

    “Simba haihujumiwi kama tunavyosikia,
    tunapataga mipango yao mingi ya ndani
    na nje ya uwanja kupitia kwa watu wao
    ambao ni rafiki zetu,lakini pia tumesikia
    jinsi wanavyowafukuza wachezaji wao
    jambo ambalo si sahihi na wanaharibu
    kabisa muelekeo wa timu, mambo ya
    hujuma yapo kwa kila timu lakini
    yanatakiwa kufanyiwa
    uchunguzi,”alifafanua kigogo huyo
    ambaye aliomba jina lake lilindwe.

    Mbali na upinzani na ushabiki wa ndani
    na nje ya uwanja, viongozi wa Simba na
    Yanga hususani wale waliopo kwenye
    kamati mbalimbali ikiwemo ya
    mashindano, usajili hata za utendaji
    wamekuwa na urafiki wa karibu na mara
    kadhaa wameonekana kwenye vijiwe
    maarufu vya Ilala na Kinondoni wakipiga
    soga na kubadilishana mawazo kwenye
    mambo mbalimbali.

    Habari za ndani ya Simba zinadai
    kwamba matokeo ya hivi karibuni
    yamesababisha mgawanyiko baina ya
    viongozi huku baadhi wakimshutumu Rais
    wa Simba, Evans Aveva kwa misimamo
    yake ya kiuongozi kwamba amekuwa
    hafanyii kazi mambo anayoshauriwa na
    baadhi ya vigogo wa Msimbazi.
    Baadhi ya viongozi wa Simba wamezuiwa
    pia kufanya mawasiliano ya moja kwa
    moja na wachezaji huku wengine
    wakizuiwa kukanyaga kambini na kwenye
    vyumba vya kubadilishia kwa madai
    kwamba wanawachanganya na kuwagawa
    wachezaji jambo ambalo linaongeza
    mwanya wa hujuma.

    Tayari Simba imewasimamisha wachezaji
    wake mahiri watatu ambao ni Amri
    Kiemba, Shaaban Kisiga na Haroun
    Chanongo kwa maelezo kwamba
    wanawachunguza kwa sababu mbalimbali
    na wakishajiridhisha watawarudisha
    ingawa uwezekano wa wachezaji hao
    kuvaa tena jezi ya Simba mwaka huu ni
    finyu.

    Mbali na Simba kudai kwamba kuna watu
    wanatumika kuhujumu ndani kwa ndani,
    sababu nyingine ambayo wamekuwa
    wakiieleza ni kwamba baadhi ya
    wachezaji wao wameanza kuchuja.
    Simba itacheza mechi ya sita kesho
    Jumamosi dhidi ya Mtibwa Sugar, mechi
    itakayofanyika Uwanja wa Jamhuri
    mkoani Morogoro ambapo viongozi wa
    Simba wametoa tahadhari kwa wachezaji
    wao kwamba endapo matokeo yakiwa
    mabaya basi wachezaji wengine
    wanaotuhumiwa watafungashiwa virago
    vyao huku benchi la ufundi likipewa
    mechi mbili kuanzia wikiendi hii
    kujirekebisha.

    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Post a Comment

    Item Reviewed: SIMBA BADO SIYO SHWARI Rating: 5 Reviewed By: Unknown
    Scroll to Top