728x90 AdSpace

  • Latest News

    Thursday, October 30, 2014

    TAMBWE ANUKIA YANGA


    MFUNGAJI Bora wa Ligi Kuu Bara msimu
    uliopita, Amissi Tambwe, kwa sasa
    anaonekana si lolote katika timu yake ya
    Simba ambapo amefunga bao moja tangu
    msimu huu uanze, lakini imebainika
    kuwa mfumo anaotumia kocha wao
    Patrick Phiri ndio chanzo cha
    kuporomoka kwa straika huyo.

    Mchezaji huyo ambaye ameanza
    kuwatamanisha baadhi ya viongozi wa
    usajili wa Yanga, ametamka kwamba
    anamalizia mechi zake mbili zilizobaki
    Simba kufunga mwaka halafu arudi kwao
    Burundi ambako anaweza kufanya
    uamuzi mgumu kutokana na vitisho
    alivyopata klabuni kwake hivi karibuni.

    Habari za ndani zinadai Tambwe ambaye
    amebakiza miezi mitano katika mkataba
    wake ameanza kujadiliwa na baadhi ya
    vigogo wa Yanga ambayo tayari ina
    wachezaji watano wa kigeni, lakini
    mtihani ni jinsi ya kumshawishi kocha
    Mbrazili Marcio Maximo.
    Hata hivyo mabosi hao wanadai watajua
    cha kufanya baada ya kumaliza mechi
    zilizosalia mwaka huu na kusikia
    tathmini ya Kocha.

    Wakati Simba
    ilipokuwa chini ya kocha, Zdravko
    Logarusic, kocha huyo alikuwa hampi
    majukumu mengi Tambwe huku kazi yake
    kubwa ikiwa ni kukaa eneo moja na
    kusubiri mipira ya kufunga ambapo
    alikuwa kitumia mifumo ya straika
    mmoja mbele 4-5-1 au 4-2-3-1.

    Lakini Phiri amempa Tambwe majukumu
    mawili ambapo anashuka kutafuta mipira
    na kupanda kufunga jambo ambalo
    limekuwa gumu kwake kumudu
    majukumu mawili kwa wakati mmoja.

    Phiri hupendelea sana kutumia mifumo
    ya 4-4-2, 4-3-3 na 3-5-2.

    Tambwe alikiri kuwa mabadiliko hayo pia
    yamechangia kiwango chake kuonekana
    kushuka kwani hawezi kufanya yote hayo
    kwa wakati mmoja. “Kila kocha ana
    mfumo wake wa ufundishaji, nilipokuwa
    chini ya Loga sikuwa na majukumu
    mengi katika timu, lakini hivi ninapewa
    majukumu mengi ambayo si rahisi
    kuyafanya kwa wakati mmoja na kuleta
    mafanikio, hivyo nalazimika kucheza
    kutokana na kocha anavyotaka,” alisema
    Tambwe.

    Tambwe pia ni miongoni mwa wachezaji
    wanaotuhumiwa kucheza chini ya
    kiwango kutokana na matokeo ya sare
    tano mfululizo huku akitajwa kuwa ni
    mmoja wa wachezaji watakaotemwa kwa
    kosa hilo ambapo yeye amesema kwamba
    yupo tayari kuondoka ili kupisha wengine
    watakaoisaidia Simba.
    “Nipo katika wakati mgumu sana kwa
    sasa, tuhuma zimezidi jambo ambalo si
    kweli, nakosa amani ndani ya timu hivyo
    sioni sababu ya kuendelea kuwepo sehemu
    ambayo maisha yangu yapo hatarini,
    maisha ya mpira ndivyo yalivyo lakini
    kwa sasa yamezidi maana imefikia hatua
    natumiwa ujumbe wa vitisho, sasa
    nasubiri nini Simba? Nataka nikapumzike
    kidogo,” alisema Tambwe
    Tambwe pia alikuwa mfungaji bora katika
    michuano ya Kombe la Kagame alipokuwa
    na timu yake ya Vital’O ya Burundi 2013
    yaliyofanyika Sudani Kusini ambapo
    alifunga mabao sita.

    Lakini Phiri, alisema hupenda kutumia
    mifumo hiyo ili timu iweze kushambulia
    zaidi na kupata mabao, pia alikiri
    wachezaji wengi wameathirika
    kisaikolojia kutokana na matokeo
    wanayoyapata.

    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Post a Comment

    Item Reviewed: TAMBWE ANUKIA YANGA Rating: 5 Reviewed By: Unknown
    Scroll to Top